Na Mwandishi wa A24tv Dodoma .
Wananchi na wafanyabiashara wametakiwa kuhakikisha wanasajili majina ya biashara wanayotumia ili kuepuka kuvunja sheria na kulinda maslahi yao.
Akizungumza katika Maonesho ya Kilimo, Afisa Usajili wa BRELA, Yusuf Mwasakafyuka, amesema ni kosa kwa mfanyabiashara kutumia jina tofauti na jina lake binafsi katika kuendesha biashara bila kulisajili rasmi.
“Mfanyabiashara haruhusiwi kutumia jina tofauti na jina lake binafsi kuendesha biashara bila kulisajili. Kwa mfano, ukifungua saluni na kuiwekea jina tofauti, unatakiwa ulisajili ndani ya siku 28. Usajili wa jina la biashara unasaidia kulinda biashara yako na kuzuia watu wengine kutumia jina hilo bila idhini.”

Mwasakafyuka ameongeza kuwa sheria inampa Msajili mamlaka ya kuchukua hatua dhidi ya anayekiuka utaratibu huo, ikiwemo kufuta usajili wa biashara husika, huku wahusika wakikabiliwa na madai endapo matumizi ya jina hilo yatasababisha hasara kwa mmiliki halali.
Amesisitiza wafanyabiashara kuzingatia sheria za usajili wa majina ya biashara ili kujiepusha na migogoro ya kisheria na kuhakikisha biashara zao zinapata ulinzi wa kisheria.

Mwisho..
