Na Mwandishi wa A24tv. Karatu
Mkuu wa Wilaya ya Karatu, Mhe. Dkt. Lameck Karanga, leo Septemba 1, 2026, amejionea zoezi la uandikishaji wa Vitambulisho vya Taifa (NIDA) kwa wananchi wa Kijiji cha Qaru, Tarafa ya Endabash, Wilaya ya Karatu.


Akiwa katika kituo cha uandikishaji, Mhe. Dkt. Karanga amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na uongozi wa NIDA kwa kuwezesha watumishi kuwafikia wananchi vijijini na kutoa huduma hiyo bila malipo.

Aidha, Mhe. Dkt. Karanga amewataka wananchi kuhakikisha wanatumia nyaraka halali na sahihi wakati wa kuwasilisha taarifa zao, hatua ambayo itasaidia kupunguza changamoto zinazoweza kujitokeza katika usajili na utoaji wa vitambulisho pamoja na namba za NIDA.
Zoezi hilo limefanyika katika Kijiji cha Qaru kwa takribani siku mbili, huku leo, Septemba 1, likiwa siku ya hitimisho.


Baada ya kukamilika kwa zoezi hilo Qaru, timu ya NIDA inatarajiwa kuendelea na zoezi hilo katika maeneo mengine yenye changamoto, hususan kuwafikia wananchi ambao bado hawana namba au Vitambulisho vya Taifa.
Mwisho.
