Na Geofrey Stephen A24tv.
“Arusha ni salama, tulivu na kivutio bora cha utalii Afrika” – RC Makalla
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. CPA Amos Gabriel Makalla, amewahakikishia usalama na utulivu washiriki wa wa kozi ya ya Ndc kundi la kumi na nne kutoka nchi 16 za Afrika na nje ya bara hilo wanaoshiriki mafunzo ya Chuo cha Taifa cha Ulinzi (National Defence College – NDC).
Akizungumza leo Jumatatu, Novemba 10, 2025, wakati wa kuwapokea washiriki wa kozi hiyo wapatao 72 katika ofisi ya Mkoa wa Arusha, CPA Makalla alisema Mkoa huo umeendelea kuwa mfano wa amani, jambo linalochochea ukuaji wa sekta ya utalii na uwekezaji.


“Mkoa wa Arusha ni Kituo Kikuu cha Utalii kwa Kanda ya Kaskazini. Nawakaribisha sana, mjisikie mpo nyumbani. Arusha inaendelea vyema katika sekta ya utalii na nyinginezo za kiuchumi, na tumeendelea kuwa salama kutokana na ushirikiano mkubwa kati ya wananchi na vyombo vya ulinzi na usalama,” alisema CPA Makalla.
Washiriki Kutoka Nchi 16
Ujumbe huo unaongozwa na Balozi Meja Jenerali Wilbert Ibuge, Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC).
Miongoni mwa nchi zinazoshiriki ni Tanzania, Kenya, Uganda, Zimbabwe, Afrika Kusini, Malawi, na Bangladesh, pamoja na nyinginezo kutoka ndani na nje ya bara la Afrika.



Mafunzo na Ziara za Kujifunza Utalii
Kupitia programu yao maalum inayojulikana kama “Tentative Programme for Economy in Tourism”, washiriki hao wanatarajiwa kujifunza kwa vitendo namna sekta ya utalii inavyochangia uchumi wa taifa.
Katika kipindi cha siku tano watakachokaa Arusha, watatembelea vivutio vya kipekee na taasisi muhimu zikiwemo:



- Makao Makuu ya TANAPA
- Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA)
- Makao Makuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC)
- Pamoja na vivutio mbalimbali ndani ya Jiji la Arusha
Ziara hizi zinalenga kuhamasisha uelewa mpana wa utalii, diplomasia, tamaduni na maendeleo ya kiuchumi katika Jiji la Arusha, mji unaotambulika kimataifa kama kitovu cha mikutano na utalii barani Afrika.
Mwisho .



