Na Mwandishi Wetu A24 Tv
Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) imeeleza kutoridhishwa kwake na utendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Same, ikiongozwa na Afisa Masuuli, kutokana na uzembe na kukosekana kwa utayari wa kushughulikia hoja za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) pamoja na maagizo ya Kamati.
Kupitia taarifa iliyosomwa Agosti 20, 2026, na Mwenyekiti wa Kamati ya LAAC, Mheshimiwa Ado Shaibu Ado (MB) wakati wa kikao cha kupitia na kuchambua Taarifa ya hesabu zilizokaguliwa za Halmashauri hiyo kwa miaka ya fedha 2023/2024 na 2024/2025, Kamati ilibainisha kuwa kiwango cha utekelezaji wa maagizo na hoja kiko chini sana.

Kiwango cha Utekelezaji wa Maagizo na Hoja
Maagizo ya Kamati (Kikao cha Oktoba 27, 2024): Kati ya maagizo 7 yaliyotolewa, ni maagizo 2 pekee (sawa na 28%) ndiyo yaliyotekelezwa kikamilifu.
Hoja za CAG (Mwaka 2024/2025): CAG alitoa hoja na mapendekezo 18, lakini Halmashauri imetekeleza hoja 4 tu (sawa na 22%). Hoja za Miaka ya Nyuma: Kati ya hoja 9 zilizotolewa na CAG kwa miaka iliyopita, Halmashauri imefanikiwa kutekeleza hoja 3 tu.
Mheshimiwa Ado Ado alieleza kuwa hali hiyo ni dharau kubwa kwa Bunge na kwa CAG, ambaye ndiye jicho la Bunge.

Kutokana na kutokutimizwa kwa wajibu huo, Kamati imesitisha mahojiano na Halmashauri ya Same na kuitaka ikatekeleze hoja zote zilizosalia.
Aidha hatua hii imetolewa kama onyo kwa Halmashauri zote nchini ambazo zimekuwa zikidharau na kuacha kutekeleza maagizo ya Kamati na hoja za CAG.
Mwisho..
